Uchaguzi Marekani 2020: Kanye West atangaza kuwania urais wa Marekani

Chanzo cha picha, Getty Images
Kanye West amesema anawania urais wa Marekani. Haifahamiki kama mwanamuziki huyo amemaanisha kweli kile alichokisema, au hiyo ni njia tu ya kutafuta kuzungumziwa tu ifahamikavyo na wengi (Kiki) limeeleza shirika la habari la Bloomberg.
Ujumbe wa Kanye uliowekwa kwenye mtandao wa Twitter siku ya Jumamosi usiku ulisambaa sana mitandaoni, huku ukirudiwa kuchapishwa mara 100,000 ndani ya kipindi cha saa nne. West ana wafuasi milioni 29.4 kwenye mtandao wa Twitter. 'Kanye' kwa haraka sana akawa ndiye anayezungumziwa zaidi kwenye mtandao huo nchini Marekani.
''Lazima sasa tutambue ahadi ya Marekani kwa kumuamini Mungu, kuunganisha maono yetu na kujenga mustakabali wetu,'' West aliandika akinukuliwa na gazeti la The Guardian.
Mkala hii imebeba madhui yaliyotoka kwenye mitandao ya kijamii. Tunaomba ruhusa yako kabla kitu chochote hakija pakiwa, sababu wanaweza wakawa wanatumia Cookies na tekinolojia nyingine. Unaweza ukasoma sera sera ya kutumia cookies katika mitandao ya kijamii kabla ya kukubali. Kutazama maudhui haya chagua accept and continue
Mwisho wa X ujumbe
Ikiwa imebaki miezi minne kabla ya kura za tarehe 3 mwezi Novemba, haijabainika kama tweet ya West ingefaa zaidi katika siku ya wajinga duniani ya mwezi Aprili kuliko siku ya maadhimisho ya uhuru wa Marekani.
Kama West alichokisema kilikuwa si cha masihara, basi kuna mlolongo mrefu wa vihunzi katika kuelekea azma hiyo, ikiwemo kuanza kampeni tangu awali mwezi Julai mwaka huu wa uchaguzi. Atahitaji kufuzu katika majimbo 50 na pia kujenga taasisi ya kisiasa kuanzia mwanzo bila usaidizi.
Kwa sasa, West hajaonekana kujaza fomu za tume ya uchaguzi nchini humo kwa ajili ya kuwania nafasi hiyo ya juu, kwa mujibu wa Bloomberg baada ya kupitia data za tume hiyo FEC,

Chanzo cha picha, Getty Images
West, 43, amezungumzia suala la kuwania urais miaka kadhaa nyuma, na mwaka jana aliiambia hadhira yake kuwa atawania urais mwaka 2014. Yeye na mkewe, Kim Kardshian West, wamefanya kazi na rais Donald Trump mara kadhaa ikiwemo wakati wa shughuli za kuwafungulia wafungwa.
West na mkewe walishawahi kumtembelea Trump kujadili mabadiliko katika magereza mwaka 2018, baada ya mkutano huo West alimsifu Trump akisema amemfanya kujihisi shujaa, akamkumbatia na kukiri: ''Ninampenda huyu mtu.''
Trump aliulizwa kama West anaweza kuwa rais siku moja ,Trump alijibu: ''Sana tu anaweza kuwa.''












